Wednesday, April 5, 2017

PROF KITILA :MIMI SIYO MWANASIASA TENA




MSHAURI wa Chama cha ACT Wazalendo, Profesa Kitila Mkumbo, ametangaza kuachana na siasa na kuwa mtumishi wa umma kwa asilimia 100.



PROFESA KITILA MKUMBO.

Jana Rais John Magufuli, alitangaza kufanya mabadiliko madogo katika safu ya Makatibu wakuu na kumteua Profesa Mkumbo kushika nafasi iliyoachwa wazi na Mhandisi Mbogo Mfutakamba, aliyekuwa Katibu Mkuu wa wizara ya Maji na Umwagiliaji.



Akizungumza na Nipashe kwa njia ya simu, Profesa Mkumbo alishukuru kwa uteuzi huo na kueleza kuwa unapopewa kazi na Mkuu wa nchi kinachopaswa ni kuwajibika kwa niaba yake.



“Nimeipokea kuwa ukipewa kazi na Mkuu wa nchi unaheshimu kazi, unaheshimu aliyekua kazi yake, unaifanya kwa bidii kadri Mungu alivyokujalia, name nitafanya hivyo,” alisema na kuongeza:



“Mimi ni mtumishi wa umma, kiutumishi rais ana mamlaka ya kuwatumia kwa kadri anavyoona, nadhani ameona nitaweza kutumikia kwenye nafasi hiyo, namshukuru Rais, Namshukuru Mungu, basi nakwenda kuitumikia,” alisema.



Kuacha siasa kwa asilimia 100



Mkumbo alipoulizwa juu ya kuwa na ‘damu’ ya siasa, alisema kuanzia sasa anasimamisha shughuli za kisiasa na kuwa mtumishi wa umma kwa asilimia 100.



“Mambo ya kisiasa kwa sasa itabidi yasimame, nimsaidie Mheshimiwa rais kuhakikisha nchi hii inapata maji  kama anavyotarajia na sera za serikali zilivyo,” alifafanua.



Aprili 17, mwaka jana, Mkumbo alikaririwa na vyombo vya habari kuwa “Huu utaratibu wa kuwateua wasomi tu ambao ni walimu na wanataaluma kutoka vyuo vikuu hasa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) si mzuri maana rais haoneshi kuwaandaa wengine kuchukua nafasi zao, tuachwe wasomi tufanye kazi za kitafiti na kitaaluma.”



Alipoulizwa juu ya kuikosoa serikali alisema “Hoja yangu kubwa ilikuwa ni kwamba serikali inapoteuwa ni lazima iajiri, lazima kuwe na ‘replacement’.”



Kitila ambaye amewahi kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema Taifa, alipoulizwa tafsiri ya uteuzi huo kwa upinzani, alisema “ni heshima kwamba mtu mmoja ambaye alikuwa mpinzani anateuliwa maana yake kuna wapinzani wenye sifa za kiutumishi.”



“Pia ni kumshukuru rais kuwa ana uwezo wa kuvuka mipaka, amevunja ile miiko kwamba ni lazima utoke chama flani. Mtu kama mimi amenipa mtihani lazima nikaishi kama mtumishi wa umma kama ambavyo taratibu na sheria zinazopaswa kuwa,” alibainisha.



Atakalosimamia



Alisema maji ndilo hitaji namba moja la Watanzania na kwamba atafanya kazi kwa bidii kuhakikisha wananchi wanapata maji kama inavyotakiwa.



Katika kundi la Whatsapp la ACT Habari, wanachama walihoji uongozi wa ACT jinsi walivyopokea uteuzi huo na kama Profesa Kitila ameupokea.



Afisa habari wa ACT wazalendo, Abdallah Khamisi, aliulizwa wameupokeaje uteuzi wa Profesa, alijibu “vuteni subira”



Zitto:Jambo zito



Aidha, Kiongozi wa ACT Wazalendo, Zitto Kabwe, katika group hilo, waandishi walitaka kusikia kauli yao (ACT), lakini akawataka watulie na alipoelezwa kuwa uchapishaji wa gazeti unakwenda na muda (deadline).



Alisema “Kwa hiyo tufanye mambo yetu kwa deadline yako (kataja jina la mwandishi)? Hili jambo zito sana.”



Septemba 03, mwaka jana, Rais Magufuli akizungumza na Wananchi wa Zanzibar, alisema “Rais uchaguliwe upate asilimia 92 bado unachukua watu wa vyama vingine unawaingiza kwenye serikali yako. Mimi nilipata asilimia 58, hakuna wa chama kingine mle ndani, na wala hataingia,”



Huku akishangiliwa na wana CCM waliohudhuria mkutano huo, alisisitiza kuwa Dk. Shein ana moyo wa tofauti “amepata asilimia 92 bado analeta wengine, mimi nimepata asilimia 58 hakuna atakayekanyaga mguu kwenye serikali yangu.Unguja Hoyee!Zanzibar Hoyee! Ndiyo maana nasema mzee huyu ana moyo wa tofauti…naomba Mungu anisaidie angalau nipate karobo ka moyo wako.”



Mnyika: Imedhihirisha alikuwa mamluki



Mjumbe wa kamati Kuu ya Chadema, John Mnyika, alisema uteuzi wa Profesa Kitila kuwa sehemu ya serikali unadhirisha ilikuwa sahihi kufukuzwa Chadema.



“Huo uteuzi umedhihirisha maamuzi yaliyofanywa na kamati Kuu ya Chadema ya kumfukuza uanachama kutokana na usaliti yalikuwa ni sahihi, kwamba alikuwa anatumika na utawala,” alibainisha Mnyika.



Mwaka 2013, Profesa Kitila, aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu, Zitto na Samson Mwigamba, walifukuzwa Chadema kwa madai ya kukiuka Katiba, sheria na kanuni za chama hicho.



Katika uteuzi huo, Rais amemteua Dk. Ave Maria Semakafu kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, akijaza nafasi iliyoachwa wazi na Dk. Leonard Akwilipo, ambaye ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo.



Kwa alipoulizwa na Nipashe, Dk. Semakafu ambaye ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), alisema hawezi kuzungumza lolote kwa kuwa bado hajapokea taarifa rasmi zaidi ya kusoma kwenye mitandao ya kijamii.



“Unajua iko kwenye mitandao mimi sina taarifa, ‘I can not comment anything’ mpaka nitakapoelezwa ni kitu gani, kila mtu ananipa hongera ila sijaelewa, naomba msubiri nipate taarifa kamili,” alisema Dk. Semakafu ambaye pia ni mwanaharakati na Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba.



Katika uteuzi huo wengine ni Dk. Akwilipo ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, na aliyekuwa Katibu Mkuu, Maimuna Tarishi, amehamishwa na kuwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge).



Kiongozi huyo anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Mussa Uledi ambaye uteuzi wake ulitenguliwa.



ZITTO ATOA NENO

CHAMA cha ACT Wazalendo, kimepokea kwa mikono miwili uteuzi wa Prof. Kitila Mkumbo kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Maji na Umwagiliaji na kwamba kimekubali barua ya kujiuzulu kwake kwenye nafasi ya ushauri wa chama.



Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma, Kiongozi wa Chama hicho ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma mjini Zitto Kabwe alisema uteuzi huo umeonesha kuwa Rais Dk. John Magufuli ameona kuwa hata watanzania walio kwenye Vyama vya Upinzani wana uwezo, weledi na uzalendo wa kutumikia nchi.



“Kwa hatua hii, tunaona Rais ameamua kuunganisha nchi yetu kwa kufanya kazi na watu wote bila kuwabagua kwa itikadi zao za vyama. Watanzania ni wamoja na kauli za kuwagawa zinaumiza zaidi Taifa kuliko kuliweka pamoja. Tunaamini kuwa Rais Ana nia njema katika uteuzi huu na sisi tumempa baraka zote Mwanachama wetu na mwanzilishi wa Chama kwenda kwenye nafasi ya juu zaidi ya utumishi wa umma,”alisema



 Alieleza anaamini hatamwangusha Rais na muhimu zaidi hatawaangusha watanzania na aitumikie nafasi hiyo kwa uadilifu, uaminifu na weledi.





Alisema kutokana na uteuzi huo Prof. Mkumbo hawezi kuendelea kuwa Mshauri wa Chama nafasi ambayo ilimfanya kuhudhuria vikao vyote vya Chama ikiwemo Kamati Kuu.



“Ndugu Mkumbo ameandika barua ya kujiuzulu nafasi yake ya mshauri wa Chama na kubaki kuwa mwanachama wa kawaida tu. Nimeipokea barua yake na kumkubalia Kwa maslahi mapana ya nchi yetu,”alisema Mbunge huyo



Alisema ni vigumu Prof.Mkumbo kukataa uteuzi kwa kuwa yeye ni mtumishi wa umma na hatua hiyo ni kama kupanda cheo kwenye utumishi.



“Prof. Mkumbo tunamshukuru kwa mchango wake katika uongozi wa Chama chetu kwa wakati wote ambao alikitumikia Chama chetu kama mshauri wa chama. Msimamo wa chama chetu ni utumishi wa kizalendo kwa Taifa utokanao na kila mwananchi,”alisema



 Alisema Wizara hiyo ni kubwa na muhimu sana kwa nchi kwa kuwa Maji ni tatizo moja kubwa ambalo wananchi wanakumbana nalo na kama Taifa halijaweza kulimaliza.



Alibainisha Katibu huyo mteule ataenda kuongeza nguvu ya kumaliza kero ya maji na kuhakikisha anaimarisha kilimo cha umwagiliaji nchi nzima na kumtaka aanze na ajenda ya Mfuko wa Maji Vijijini na kuanzishwa Kwa Wakala wa Maji Vijijini utakaosimamia upatikanaji wa maji kwa wananchi.



Alipoulizwa kama uteuzi huo utakidhoofisha Chama hicho, Kabwe alisema watu wamekuwa na tafsiri nyingi kuhusu uteuzi huo wengine wakidai utadhoofisha chama au kufutwa machozi na kwamba chama hakiwezi kulinyima Taifa mtu mwenye uwezo na weledi.



“Tulichojiuliza tunalinden chama au tulinde nchi tukaona hatuwezi kuwanyima watanzania mtu kama Kitila aende kuwatumikia,”alisema Kiongozi huyo

No comments:

Post a Comment