Monday, April 3, 2017

Yanga mbabe wa Azam baada ya misimu mitatu



Yanga ilipata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Azam FC juzi Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, ilikuwa ni mechi ya Ligi Kuu Tanzania Bara inayoendelea.

Umekuwa ni ushindi wa kwanza kwa mabingwa hao watetezi baada ya misimu mitatu.

Yanga ilikuwa haijaifunga Azam kwenye mechi za Ligi Kuu tangu msimu wa 2013/14.

Mara ya mwisho timu hiyo kuifunga Azam ilikuwa ni Februari 23, 2013, ikiwa ni Ligi Kuu msimu wa 2012/13.

Yanga ilishinda bao 1-0 lililofungwa na Haruna Niyonzima dakika ya 32 na baada ya hapo, timu hizo zimecheza mechi nane matokeo yakiwa ni ushindi kwa Azam au sare.

Kwenye mechi ya ligi ndipo Yanga ilipopata tena ushindi wa bao 1-0 lililofungwa na Obrey Chirwa dakika ya 70.

Rekodi zinaonyesha kuwa timu hizo zimekutana mara 18 sasa, tangu Azam ilipoanza kucheza Ligi Kuu msimu wa 2008/09.

Azam imefanikiwa kushinda mara sita, Yanga ikishinda mara tatu huku zikitoka sare mara saba.

Zifuatazo ni rekodi zinazoonyesha matokeo ya mechi za Ligi Kuu, kuanzia pale Yanga iliposhinda mechi kwa mara ya mwisho dhidi ya Azam FC.

Yanga 1-0 Azam (2012/13)
Ilikuwa ni Februari 23, 2013, Yanga iliposhinda bao 1-0 lililofungwa na Haruna Niyonzima na baada ya hapo, ikawachukua misimu mitatu kushinda tena.

1. Yanga 2-3 Azam (2013/14)
Yanga ilichapwa mabao 3-2 dhidi ya Azam FC kwenye mechi ya mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu msimu wa 2013/14, Septemba 22, 2013.

Mabao ya washindi yalifungwa na John Bocco, Kipre Tchetche, na Joseph Kimwaga, huku ya Yanga yakifungwa na Didier Kavumbavu na Hamisi Kiiza.

2. Yanga 1-1 Azam (2013/14)
Mechi ya mzunguko wa pili msimu huo huo, iliisha kwa sare ya bao 1-1.

Mechi ilichezwa Machi 19, 2014 mabao yakifungwa na Didier Kavumbagu na la Azam likifungwa na Kelvin Friday.

3. Yanga 2-2 Azam (2014/15)

Timu hizo zilitoka sare ya mabao 2-2 mechi ya kwanza msimu wa 2014/15.

Ilikuwa ni Desemba 28, 2014 mechi hiyo ilipochezwa, Amissi Tambwe na Simon Msuva wakiifungia

Yanga, huku Didier Kavumbagu ambaye alikuwa ameshatoka Yanga na kujiunga na Azam akiipatia bao, Bocco pia akifunga lingine.

4. Yanga 1-2 Azam (2014/15)
Ilikuwa ni Mei 6, 2015, mechi ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu msimu huo huo, Yanga ilipoangukia pua kwa kuchapwa mabao 2-1 dhidi ya Azam.

Rafael Brayson na Aggrey Morris waliifungia Azam, huku Andrey Coutinho akifunga bao la kufutia machozi kwa Yanga.

5. Yanga 1-1 Azam (2015/16)
Ilikuwa ni sare ya bao 1-1 Ligi Kuu msimu uliopita, Oktoba 17, 2015 kwa mabao ya Donald Ngoma kwa Yanga na Kipre Tchetche kwa Azam FC.

6. Yanga 2-2 Azam (2015/16)
Ni mechi ya mzunguko wa pili msimu uliopita, timu hizo zikitoka sare ya mabao 2-2, mawili ya Juma Abdul akijifunga na kuipatia Yanga bao.

Mengine kwenye mechi hiyo iliyochezwa Machi 5, mwaka jana yalifungwa na Bocco kwa Azam na Ngoma kwa Yanga.

7. Yanga 0-0 Azam (2016/17)
Ni mechi ya kwanza msimu huu, ikichezwa Oktoba 16, na kutoka sare ya bila kufungana.

8. Yanga 1-0 Azam (2016/17)
Chirwa alifunga bao pekee Aprili Mosi na kuhitimisha ukame wa ushindi kwa Azam kwa misimu mitatu mfululizo.

No comments:

Post a Comment